VITUS BENEDICTO MTAFYA

SPORT AND GAMES

Thursday, June 18, 2015

Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema, Freeman Mbowe AHUKUMIWA Jela Mwaka Mmoja au kulipa faini ya Sh milioni moja.


MAHAKAMA ya wilayani Hai mkoani Kilimanjaro, imemtia hatiani na kumhukumu Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema, Freeman Mbowe kwenda jela mwaka mmoja au kulipa faini ya Sh milioni moja, kutokana na kesi iliyokuwa ikimkabili ya kumshambulia mwangalizi wa ndani wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010.
 
Akisoma hukumu hiyo iliyohudhuriwa na wabunge wengi wa Chadema, Hakimu Mkazi Mfawidhi, Denis Mpelembwa, alisema mahakama imemkuta Mbowe na hatia, hivyo kutakiwa kutumikia kifungo cha mwaka mmoja jela au kulipa faini kiasi cha Sh milioni moja.
 
Mbowe ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Hai, katika kesi hiyo ya jinai namba 73 ya mwaka 2011, alidaiwa kumshambulia Nassir Yamin, katika Kijiji cha Nshara, kata ya Machame Kaskazini, Wilaya ya Hai, katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010. 
 
Mpelembwa alisema mahakamani hapo kuwa hukumu iliyotolewa mahakamani hapo imezingatia ushahidi uliotolewa kwa upande wa mlalamikaji Nassir Yamini.
 
Kwa upande wake, Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe akizungumza mahakamani hapo, alisema hukumu iliyosomwa mahakamani hapo haijamtendea haki.
 
Alisema kesi yake hiyo haikustahili kuchukua muda mrefu kama mahakama ilivyofanya kwa kuchukua zaidi ya miaka mitano bila kusomewa hukumu.
 
Hata hivyo, Mbowe amelipa kiasi cha fedha Sh milioni moja alichotakiwa kulipa kama hukumu ilivyoeleza, kwa kumtaka kulipa kiasi hicho cha fedha au kwenda jela mwaka mmoja.

No comments: