VITUS BENEDICTO MTAFYA

SPORT AND GAMES

Tuesday, March 17, 2015

watu wawili wafariki mbeya







Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya,SACP Ahmed Msangi.
Akithibitisha kutokea kwa matukio hayo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Ahmed Msangi amesema katika tukio la kwanza Mwili wa marehemu ulikutwa katika nyumba aliyokuwa akiishi mnamo tarehe 16.03.2015 majira ya saa 10:00 asubuhi huko katika kitongoji cha rusungo, kijiji na kata ya chitete, tarafa ya bulambya, wilaya ya ileje, mkoa wa Mbeya.
Mwili wa marehemu ulikutwa ukiwa na majeraha sehemu za kichwani ya kukatwa kitu chenye ncha kali na huku ukiwa umeanza kuharibika. chanzo cha tukio hilo kinachunguzwa, upelelezi zaidi unaendelea ikiwa ni pamoja na kuwatafuta watu waliohusika katika tukio hili.
Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya kamishna msaidizi mwandamizi wa polisi Ahmed z. Msangi anatoa wito kwa yeyote mwenye taarifa zitakazosaidia kupatikana kwa watu waliohusika katika tukio hili azitoe katika mamlaka husika ili wakamatwe na hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao.
Mwanafunzi wa kidato cha tatu katika shule ya sekondari kiwira wilayani Rungwe aliyefahamika kwa jina la Yohana Kaini (17) mkazi wa kijiji cha ibula alifariki dunia baada ya kugongwa na gari ambalo halikuweza kufahamika namba zake za usajili wala dereva wake.
Tukio hilo limetokea mnamo tarehe 16.03.2015 majira ya saa 07:00 asubuhi huko katika kitongoji cha kikumbe, kijiji cha Ibula, kata ya Kiwira, tarafa ya Ukukwe, wilaya ya Rungwe, mkoa wa Mbeya.
Inadaiwa kuwa, marehemu akiwa na mwanafunzi mwenzake aitwaye Rojas Yusuph (15) mkazi wa kijiji cha ibula wakiwa wamepakizana kwenye baiskeli wakielekea shule ndipo waligongwa na gari hilo lililokuwa likitokea tukuyu kuelekea mbeya mjini.
Katika ajali hiyo Rojas Yusuph alijeruhiwa na amelazwa katika hospitali ya misheni Igogwe-Tukuyu. chanzo cha ajali ni mwendo kasi. dereva alikimbia mara baada ya ajali na juhudi za kumtafuta zinaendelea.
kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya kamishna msaidizi mwandamizi wa polisi Ahmed Z. Msangi anatoa wito madereva kuwa makini wanapotumia vyombo vya moto ikiwa ni pamoja na kufuata sheria na alama za usalama barabarani ili kuepuka ajali. aidha anatoa wito kwa yeyote mwenye taarifa za mahali alipo dereva wa aliyesababisha ajali hii azitoe katika mamlaka husika ili akamatwe na hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yake.

No comments: